728x90 AdSpace

  • Latest News

    Wednesday, December 30, 2015

    Polisi ahukumiwa maisha jela Ilala Dar es salaam

    Mahakama ya Wilaya ya Ilala imemhukumu, kifungo cha maisha jela, polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, PC Daniel (24), baada ya kupatikana na hatia ya kubaka na kumlawiti mtoto wa kike mwenye umri wa miaka 13.

    Mbali ya hukumu hiyo, pia Mahakama hiyo imemtaka mshtakiwa huyo kulipa faini ya Sh2 milioni kwa mtoto huyo.

    Akitoa hukumu hiyo jana, Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Ilala, Said Mkasiwa alisema PC Daniel atatumikia kifungo cha maisha jela baada ya mahakama kuridhishwa na ushahidi uliotolewa na mashahidi wanne wa upande wa mashtaka.

    Mkasiwa alisema kuwa baada ya mahakama kusikiliza mashahidi hao, ilimwona mshtakiwa kuwa na kesi ya kujibu na ilimtia hatiani kwa mashtaka mawili. Katika shtaka la kwanza, mshtakiwa alihukumiwa kifungo cha miaka 30 jela; na katika shtaka la pili kifungo cha maisha jela.

    “Mahakama inakutia hatiani. Hivyo, ninakuhukumu kifungo cha maisha jela na kumlipa mlalamikaji fidia ya shilingi milioni mbili ili liwe fundisho kwa vijana wengine ambao wanazijua vizuri sheria lakini bado wanazivunja,” alisema Mkasiwa.

    Kabla ya kutolewa kwa hukumu hiyo, Wakili wa Serikali, Erick Shija aliiomba Mahakama kutoa adhabu kali kwa askari huyo ili liwe fundisho kwa watu wote wanaofanya vitendo vya kikatili kama hivyo.

    Lakini Manze, wakili aliyekuwa anamtetea askari huyo aliiomba Mahakama kumpunguzia adhabu mteja wake kwa sababu ni kosa la kwanza na kwamba alifanya tukio hilo alipokuwa anatoka kwenye starehe na kwamba chanzo chake ni pombe.

    Hata hivyo, baada ya kusikiliza hoja hizo, hakimu Mkasiwa alimtia hatiani askari huyo na kumhukumu kifungo cha maisha jela na kulipa faini hiyo.

    Kwa mujibu wa hati ya mashtaka, askari huyo anakabiliwa na mashtaka mawili ya kubaka na kulawiti. Katika shtaka la kwanza, mshtakiwa alidaiwa kutenda kosa la kumbaka mtoto huyo wa kike mwenye umri wa miaka 13 eneo la Tabata Maduka Mawili, wilayani Ilala.

    Katika shtaka la pili, siku hiyohiyo na eneo hilohilo, mshtakiwa huyo alidaiwa kumlawiti mtoto huyo wa kike na hivyo kumsababishia maumivu sehemu zake zote za siri.

    Baada ya kutenda makosa hayo, mshtakiwa inadaiwa alikimbia na baadaye alikamatwa mkoani Tanga, Februari na akarejeshwa kukabili mashtaka dhidi yake
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Post a Comment

    Item Reviewed: Polisi ahukumiwa maisha jela Ilala Dar es salaam Rating: 5 Reviewed By: Unknown
    Scroll to Top