728x90 AdSpace

  • Latest News

    Tuesday, August 25, 2015

    MDOMO WA JULIO HAUWEZI UKAFUTA SIFA ZAKE KAMWE.

     
    NIKO kwenye jiji kubwa kuliko yote hapa nchini Uturuki. Mengi yanaweza yakawa yanajulikana au gumzo, lakini huenda hakuna zaidi ya soka.

    Si unajua Tanzania tunavyopenda soka la England na tunashangilia kwelikweli huku kila mtu akiwa amejipandika timu yake, hapa sahau.
    Wao wana timu zao, wanaziheshimu na kuzipa thamani kubwa kuliko unavyofikiria. Mambo ya England, wamewaachia Waingereza wenyewe.
    Hii pia ni kutokana na kukua kwa soka la hapa ambalo linatawaliwa na klabu kubwa tatu za Galatasaray, Fernabahce pamoja na Beskats.
    Soka lao, kweli linapiga hatua. Mambo wanayofanya yamenifanya nikumbuke nyumbani kwa kuwa nilimsikia Kocha Mkuu wa Mwadui FC, Jamhuri Kihwelo ‘Julio’ akijitamba kabla ya mechi yake ya kirafiki dhidi ya Simba.

    Halafu baada ya sare, akakumbushia alichokisema kwamba timu yake yenye wazalendo wengi ina uwezo mkubwa.
    Kweli wameisumbua Simba na kumaliza mechi kwa sare ya bila mabao. Naweza kusema, acha tumsubiri Julio katika Ligi Kuu Bara.
    Pamoja na hivyo, sikuishia hapo. Muungwana yoyote angependa kujipa maswali na ikiwezekana kuyajibu kwa haki bila ya kuonea.,
    Hivi huyu Julio, kweli tunapaswa kuamini sifa yake moja tu, kwamba ni mtu wa maneno mengi sana, kelele nyingi sana na hana lolote.
    Pamoja na maneno yake ambayo huenda ni asili kwake kwa kuwa amekulia uswahilini kama kwetu, kule Kigogo jijini Dar es Salaam, lakini kazi yake mbona inaonekana.
    Aliipandisha Mwadui FC msimu uliopita kwa maana ya pointi, akaachwa daraja la kwanza kwa kuwa Stand United walikata rufaa na kushinda.
    Ungesema hesabu ni uwanjani basi yeye alistahili kusonga mbele. Ok, akaapa msimu unaofuatia atapanda.
     
    MWADUI FC
    Kweli msimu uliofuatia Mwadui FC ikapanda, tena ikabeba na ubingwa wa daraja la kwanza kwa kuifunga African Sports.
    Usisahau wakati anaipandisha timu, asilimia kubwa ya wachezaji aliokuwa nao ni wale walioonekana hawafai kwenye vikosi vingi, mfano mzuri ni Athumani Iddi ‘Chuji’ ambaye alimpa unahodha kabisa.
    Hali inavyokwenda, Julio anakwenda kuwa tishio Ligi Kuu Bara kama hatayumba kupitia mwendo anaokwenda.
    Julio ni Mtanzania, pamoja na maneno yake, kazi yake bora kabisa inaonekana. Lakini karibu kila mmoja ametia pamba machoni na vipanzi masikioni asisikie wala kuona mazuri anayofanya.
    Waturuki wanathamini na kutamani vyao. Hatumpi Julio sifa yake lakini Wazungu wanakuja nyumbani kwetu, wanalipwa mara tatu nne au tano ya Julio na hawafanyi kama kazi yake.
    Niliwahi kukumbusha kuhusiana na Julio, kweli ana maneno mengi, kweli ana shombo. Lakini huyu jamaa ni muhimu sana katika mpira wa Tanzania.
    Ana ya kumlaumu au anaudhi lakini ni changamoto, hakika anaupenda mpira kwa dhati na ndiyo maisha yake miaka yote.

    Sina haja yoyote ya kutaka kulaumu, lakini nataka niwakumbushe kwamba huyu Julio tumthamini, tumkubali na tumpongeze kwa kuwa Mtanzania mchapakazi na mwenye mafanikio kwa mengi anayoyafanya kwenye mpira wa Tanzania.
    Tusisubiri siku ‘akishaondoka’, basi kila mmoja wetu aanza kusambaza sifa zake huku akieleza mengi mazuri kuhusu yeye.

    Hapa Uturuki wanavipenda na kuthamini vyao kwelikweli. Lakini huko nyumbani, hatupendani, hatupendi vyetu na tunapenda ugeni wa kila kitu ili mradi kiwe kinatokea nje ya mipaka ya nchi yetu!

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Post a Comment

    Item Reviewed: MDOMO WA JULIO HAUWEZI UKAFUTA SIFA ZAKE KAMWE. Rating: 5 Reviewed By: Unknown
    Scroll to Top